Powered By Blogger

Tuesday, November 8, 2011

Msajili azitaka nchi za EAC ziiamini mahakama

MSAJILI wa Mahakama ya Afrika Mashariki (EACJ), Dk. John Ruhangisa ametoa mwito kwa nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) kujenga imani kwa mahakama hiyo ili kuiwezesha kushughulikia ukiukwaji wa haki kikamilifu.

“Kutokana na uchunguzi unaofanywa ni wazi kwamba baadhi ya wadau hawatambui nafasi muhimu iliyopewa mahakama hii na Mkataba uliounda Jumuiya hii,’’ alisema Jaji Ruhangisa.

Msajili huyo wa EACJ alikuwa akizungumza na wajumbe wa warsha ya kwanza juu ya majukumu ya EACJ katika kuukuza mtangamano wa nchi wanachama, mjini Kampala nchini Uganda juzi.

Warsha hiyo, yenye kauli mbiu ‘Jukumu na nafasi ya Mahakama katika ajenda ya mtangamanao wa EAC’, ilihudhuriwa na majaji wakuu kutoka nchi wanachama, wabunge wa Bunge la EAC, wasajili wa mahakama za kitaifa, wakuu wa taasisi za EAC na wajumbe wa asasi za kiraia.

Ruhangisa alihadharisha kwamba mahakama hiyo isionekana kama ni wapinzani kila inapotoa uamuzi usiowafurahisha watunga sera.

“Mahakama inatoa tafsiri na kutumia vifungu vya sheria kutoka katika Mkataba ili kufikia malengo ya EAC na siyo kwa lengo la kumfurahisha mdau anayeguswa na uamuzi wa mahakama,” alifafanua.

Waziri Mkuu wa Kwanza na Waziri wa Masuala ya Afrika Mashariki wa Uganda, Eriya Kategaya, alisema katika warsha hiyo kwamba kadiri Itifaki ya EACJ inavyokaribia kukamilishwa, nchi wanachama hazina budi pia kuwa tayari kuachia sehemu ya mamlaka za mahakama zao za kitaifa kwa ajili ya mahakama hiyo ya Kanda.

“Ni dhahiri kwamba nchi wanachama zitachambua sheria zake za kitaifa zinazohusiana na uongozi wa mahakama na kuzioanisha na za EACJ pindi Itifaki ya mahakama hiyo ya Kanda itakapokamilika,’’ alifafanua Kategaya. Chanzo Habari leo.

No comments: