Powered By Blogger

Monday, June 27, 2011

Rufani ya Mahita yatupiliwa mbali.

MKUU wa zamani wa Jeshi la Polisi Nchini, Omar Mahita, ameumbuka kwa mara nyingine baada ya Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, kutupilia mbali rufaa yake ya kupinga hukumu ya Mahakama ya Wilaya ya Kinondoni, kuhusu sakata la mtoto anayemkataa.

Rufaa hiyo ya Mahita ilitupiliwa mbali jana na Jaji Dk Fauz Twaib, baada ya kuridhika na hukumu ya mahakama ya chini kuwa ilikuwa sahihi na kumwamuru Mahita kulipa gharama za kesi hiyo.Hata hivyo wakati hukumu hiyo ikitolewa, Mahita hakuwapo mahakamani na wakili wake Semgalawe, alifika wakati tayari jajiakiwa ameshamaliza kusoma hukumu.
 Septemba mwaka 2009 Mahakama ya Kinondoni  ilimwamuru Mahita kutoa kiasi cha Sh100,000 kila mwezi kwa ajili ya kumhudumia mtoto  na kulipa malimbikizo ya gharama za matunzo kuanzia mwaka 2003 hadi siku ya hukumu.

Hukumu hiyo ilitokana na kesi ya msingi iliyofunguliwa katika mahakama hiyo na aliyekuwa mfanyakazi wa Mahita, Rehema Shabani, kupitia kwa Kituo cha Msaada wa Kisheria na Haki za Binadamau (LHRC).Katika kesi hiyo, Rehema alikuwa anadai matunzo ya mtoto Juma Omar Mahita, baada ya kumtelekeza na baadaye mahakama ilifikia uamuzi wa kumtaka Mahita kulipa gharama hizo.Mahakama pia iliamuru Mahita akachukuliwe vipimo vya vinasaba (DNA) lakini Mahita akakataa.

Hata hivyo Mkuu huyo wa zamani wa Polisi, kupitia kwa wakili wake Charles Semgalawe aliamua kukata rufaa katika Mahakama Kuu ya Tanzania, akipinga hukumu na adhabu hiyo.Katika rufaa hiyo, Mahita aliwasilisha sababu nne za kupinga hukumu na adhabu hiyo.Alidai kuwa pamoja na mambo mengine,mahakama ya chini ilikosea kisheria kuamua kwa kuwa shauri la matunzo ya mtoto halikufunguliwa nje ya wakati, kinyume cha Sheria ya Kuasili Watoto.

Pia alidai kuwa mahakama ya chini ilikosea kusema kuwa mrufani ni baba halali wa mtoto kwa kuegemea katika ushahidi wa mjibu rufani kwa madai kuwa mrufani alikataa kuchukua vipimo vya DNA wakati si kweli.

Mahita pia alihoji uhalali wa amri ya mahakama ya chini kumwamuru kumlipa mjibu rufani kiasi Sh100,000 kila mwezi kwa ajili ya matunzo ya mtoto wakati sheria inataja kiasi cha Sh100.

Hali kadhalika, alilalamikia amri ya mahakama ya chini ya kumtaka kulipa fidia kuanzia mwaka 2003  hadi siku ya hukumu.Hata hivyo katika hukumu yake jana Jaji DK Twaib alitupilia mbali sabababu hizo  baada ya kuziona kuwa hazina msingi na kuungana na baadhi ya hoja za wakili wa mlalamikaji, Fredrick Mkatambo kutoka LHRC.


Wakili huyo alizipinga vikali sababu hizo wakati wa usikilizwaji wa rufaa hiyo.Jaji Dk Twaib alichambua sababu moja baada ya nyingine na kuzitolea maelezo ya kisheria ya sababu za kuzitupila mbali.

No comments: