Wednesday, August 8, 2012
Hukumu ya Mahalu kutolewa leo.
| Prof.Mahalu akiwa na Mawakili wake(Maktaba) |
Hakimu
Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam, Ilvin Mgeta leo
anatarajiwa kutoa hukumu ya kesi Na.1/2007 inayomkabili aliyekuwa Balozi wa
Tanzania nchini Italia, Profesa Costa Mahalu na aliyekuwa Mkuu wa Fedha na
Utawala katika ubalozi huo, bi. Grace Martin, wanaokabiliwa na kesi ya uhujumu
uchumi na kuisababishia Serikali hasara.
Hukumu
hiyo ambayo awali ilikuwa imepangwa kusomwa tarehe 10 Juali mwaka huu,
iliahirishwa na sababu zikitajwa na
Hakimu Aloyce Katemana kuwa ni Hakimu aliyekuwa asome hukumu hiyo, Ilvin Mgeta
alipata dharura na hivyo hukumu hiyo ilisogezwa mbele kusubiri atakaporejea.
Kesi hiyo
hiyo ambayo imedumu mahakamani hapo kwa miaka saba sasa, ilifunguliwa kwa mara
ya kwanza mahakamani hapo Januari 22 mwaka 2007.
Serikali yaridhia mabadiliko Sheria ya Mafao
![]() |
| Picha ya mzee kutoka Maktaba |
SIKU moja baada ya Bunge
kupitisha azimio la kutaka kuwasilishwa kwa Muswada wa Marekebisho ya Sheria ya
Mifuko ya Hifadhi ya Jamii, ambao kipengele cha muda wa ukomo wa kuchukua mafao
kimekuwa kikipingwa na wadau, Serikali imekubali ombi hilo.
Juzi, jioni Mbunge wa Kisarawe,
Seleman Jafo (CCM), aliwasilisha maelezo binafsi akitaka muswada huo urejeshwe
bungeni ili ufanyiwe marekebisho.
Jafo alitaka kupitishwa kwa
azimio ili sheria hiyo irejeshwe bungeni na kufanyiwa mabadiliko ya kifungu cha
muda wa ukomo wa kuchukua mafao ya mteja kutoka cha sasa, ambacho ni kati ya
miaka 55 hadi 60 na kisha kimruhusu mwanachama kuchukua fao la kujitoa kabla ya
umri rasmi wa kustaafu.
Akiwasilisha bungeni Makadirio ya
Mapato na Matumizi ya wizara yake kwa mwaka 2012/2013 bungeni jana, Waziri wa
Kazi na Ajira, Gaudensia Kabaka alisema sheria hiyo imepokewa kwa hisia tofauti
na umma na kutangazwa kwa hisia tofauti na vyombo mbalimbali vya habari.
Waziri Kabaka alisema baadhi ya
vyombo vya habari vilidai kuwa Serikali, iliweka kifungu cha kufuta fao la
kujitoa kutokana na mifuko mingi ya jamii kuwa katika hali mbaya kifedha.
“Wengine walisema NSSF (Mfuko wa
Taifa wa Hifadhi ya Jamii) iko hatarini kufilisika baada ya Serikali kushindwa
kulilipa shirika hilo kutokana na uwekezaji mbaya uliofanywa,” alisema Kabaka.
Kabaka alisema wapo waliodai kuwa
hatua hiyo ya Serikali ina lenga kutunisha mifuko ya hifadhi ya jamii ili
baadaye ichukue fedha hizo kwa ajili ya chaguzi mbalimbali.
Alisema sababu zote hizo hazikuwa
sahihi na kwamba Serikali inachokiona ni kuwa haikutoa elimu ya kutosha kabla
ya kuwasilisha muswada huo wa sheria Aprili, mwaka huu.
“Serikali imesikia malalamiko ya
wafanyakazi na hoja za wabunge na kuzingatia yote yaliyopo katika azimio la
Bunge na imekubali kuleta muswada kwa hati ya dharura,” alisema Kabaka.
Kamati ya Bunge ya Maendeleo ya
Jamii, imeishauri Serikali kuirekebisha sheria hiyo haraka kwa vile imeleta
mtafaruku mkubwa kwa wafanyakazi.
Akiwasilisha maoni ya kamati
hiyo, Mbunge wa Nkenge, Assumpter Mshama alisema imebaini kuwa sheria mpya
ilianza kutumia hata kabla ya kutungwa kwa kanuni zake.
Kutokana na upungufu huo, kamati
hiyo imependekeza kurejeshwa kwa fao la kujitoa na mwanachama aruhusiwe kutumia
sehemu ya mafao yake ya uzeeni kulipia mkopo wa nyumba.
Kamati hiyo imependekeza
kufanyiwa marekebisho kwa sheria hiyo ili mwanachama aruhusiwe kutumia sehemu
ya mafao yake ya uzeeni kwa ajili ya kugharimia shughuli nyingine yoyote kwa
lengo la kuandaa mazingira mazuri ya maisha baada ya kustaafu.
Kuwasilishwa kwa maelezo binafsi
ya Jafo yaliyosababisha Bunge kupitisha azimio lake juzi jioni na maelezo ya
Waziri Kabaka kulizima mjadala mkali uliotarajiwa kuibuka bungeni hiyo jana.
Wabunge wengi walikuwa wamepanga
kukwamisha bajeti ya wizara hiyo endapo Serikali ingeshikilia msimamo wake wa
kukataa kuleta muswada huo bungeni katika Bunge lijalo.
Sheria hiyo iliibua chuki na
hasira za wafanyakazi nchi nzima, huku baadhi ya vyama vya wafanyakazi
vikijiandaa kuendesha maandamano na migomo nchi nzima kupinga sheria hiyo. Chanzo gazeti la Mwananchi.
Monday, August 6, 2012
NAIBU JAJI MKUU KENYA ATIWA HATIANI.
![]() |
| Bi. Nancy Baraza |
Jopo maalum la majaji
lililoteuliwa na rais Mwai Kibaki kuchunguza tuhuma zilizokuwa zinamkabili
Naibu Jaji Mkuu wa Kenya Nancy Baraza kumdhalilisha mlinzi mmoja katika duka
moja kubwa mjini Nairobi, imependekeza, jaji huyo kuondolewa madarakani.
Akisoma hukumu hiyo mjini Nairobi
leo, mwenyekiti wa jopo hilo, Jaji mkuu mstaafu wa Tanzania, Augustino
Ramadhan, amesema Nancy Baraza akiwa mtumishi wa chombo cha kusimamia sheria na
haki hakutakiwa kwa namna yoyote kutenda kosa hilo dhidi ya mlalamikaji Bi Rebecca
Kerubo.
Amesema kitendo alichofanya Nancy
Baraza na ni cha utomvu mkubwa wa nidhamu na hivyo kupendekeza kwa Rais Mwai
Kibaki kumwondoa katika wadhifa wake wa naibu jaji mkuu.
Nancy Baraza alituhumiwa
kumnyanyasa na kumpiga Bi Kerubo tarehe 31 Desemba 2011, baada ya kutakiwa
kufanyiwa ukaguzi kabla ya kuingia katika duka hilo, utaratibu ambao umekuwa
ukitekelezwa kwa wateja wote.
Saturday, August 4, 2012
JOHN MNYIKA APELEKA MUSWADA BINAFSI WA: MAREKEBISHO YA SHERIA ZA HIFADHI YA JAMII
| Mh. John Mnyika(Mb) |
Jana tarehe 03 Agosti 2012 kwa mujibu wa Kanuni ya 68 (7) ya Kanuni za Kudumu za
Bunge na kwa kuzingatia kuwa marekebisho yamefanyika kwenye ratiba ya bunge
ambapo Mkutano wa Bunge sasa umepangwa kuahirishwa tarehe 16 Agosti 2012 na
hoja za wabunge zimeondolewa kwenye ratiba.
Nimeomba
muongozo ama Serikali itoe kauli bungeni ya kutengua tangazo lililotolewa na
Mamlaka ya Usimamizi na Udhibiti wa Sekta ya Hifadhi ya Jamii (SSRA) ili
kuwezesha mafao ya kujitoa kuendelea kutolewa au uongozi wa Bunge uruhusu
niwasilishe muswada binafsi wa sheria kwa hati ya dharura tarehe 16 Agosti 2012
kwa ajili ya kufanya marekebisho kwenye sheria husika ili kuruhusu mafao ya
kujitoa kuendelea kutolewa.
Pamoja na
hatua hiyo ya kuomba muongozo nimechukua hatua ya ziada ya kumwandikia Katibu
wa Bunge kumweleza kusudio la kuwasilisha Muswada Binafsi juu ya Marekebisho ya
Sheria za Hifadhi ya Jamii (The Social Security Laws (Ammendments) Act wa mwaka
2012 kwa hati ya dharura kwa mujibu wa Kanuni ya 81 ya Kanuni za Kudumu za
Bunge (Toleo la Mwaka 2007).Lengo la
Muswada huo ni kufanya marekebisho yenye kuwezesha kurejeshwa kwa fao la
kujitoa (withdrawal benefits) ili kuruhusu kuendelea kutolewa kwa mafao kwa
mwanachama wa mfuko ya hifadhi ya jamii anapoacha kazi na kuhitaji kupewa mafao
yake kabla ya kufikisha umri wa kustaafu kwa hiari (miaka 55) au kwa lazima
(miaka 60) au pale anapopata ulemavu wa kudumu.
Nimeomba
kupatiwa ushauri na usaidizi wa kisheria kwa mujibu wa Kanuni ya 21 (1) (d),
(e) na (2) ili kuweza kuandaa Muswada Binafsi wa Sheria kwa mujibu wa Kanuni ya
81 (1), Taarifa ya Muswada huo kwa mujibu wa Kanuni ya 81 (2), hati ya
kuwasilisha muswada kwa dharura na hoja ya kutengua masharti kuhusu muda wa
utangazaji wa Miswada ya Sheria kwa mujibu wa Kanuni ya 81 (5) ya Kanuni za
Kudumu za Bunge (Toleo la Mwaka 2007).
Kwa
mujibu wa Kanuni ya 81 (5) masharti kuhusu muda wa utangazaji wa Miswada ya Sheria
yanaweza kuwekwa kando na kutenguliwa kwa hoja kutolewa na kuamuliwa kama
kutawasilishwa Bungeni hati iliyowekwa saini na theluthi mbili ya Wajumbe wote
wa Kamati kama ni Muswada wa Kamati na kwa Muswada wa Mbunge hati iliyowekwa
saini na Wabunge wasiopungua kumi inayoeleza kuwa muswada binafsi uliotajwa
katika hati hiyo ni wa dharura.
Naomba
kutoa taarifa kwamba kuanzia jumatatu tarehe 6 Agosti 2012 nitaanza kukusanya
saini za wabunge wanaounga mkono kuwasilishwa kwa muswada tajwa kwa hati ya
dharura kufanya haraka marekebisho yenye kuwezesha kurejeshwa kwa fao la
kujitoa (withdrawal benefits) ili kuruhusu kuendelea kutolewa kwa mafao kwa
mwanachama wa mfuko ya hifadhi ya jamii.
Nimeomba
pia kwa Katibu wa Bunge kwa mujibu kifungu cha 10 cha Sheria ya ya Haki, Kinga
na Madaraka ya Bunge Cap 296 R.E 2002 kupatiwa nakala ya taarifa na nyaraka
zifuatazo kwa ajili ya kujiandaa kuwasilisha muswada husika: Social Security
Ammendment Act no.5 ya mwaka 2012, Sheria za Hifadhi ya Jamii zinazohusika,
Taarifa na mapendekezo yaliyowasilishwa na kupelekea kufutwa kwa mafao ya
kujitoa (withdrawal benefits) na maelezo kuhusu hatua ambayo kifungu husika
kiliingizwa na hatimaye kupitishwa na Bunge tarehe 13 Aprili 2012.
Pamoja na
kuomba taarifa na nyaraka kupitia kwa Katibu wa Bunge natoa mwito kwa wadau wa
mifuko ya hifadhi ya jamii kutunipatia maoni na mapendekezo kwa ya kuzingatiwa
kwenye Muswada Binafsi wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria ya Sheria za Hifadhi
ya Jamii (The Social Security Laws (Ammendments) Act wa mwaka 2012 katika
kipindi cha wiki moja.
Ikumbukwe
kwamba kifungu cha kufuta mafao ya kujitoa kilichozua mgogoro hakikuwepo wakati
muswada uliposomwa kwa mara ya kwanza bungeni tarehe 1 Februari 2012 bali
kiliwasilishwa kupitia jedwali la marekebisho ya Wizara lililowasilishwa tarehe
13 Aprili 2012 bila malengo na madhumuni yake kuelezwa kwa ukamilifu.
Kupitishwa
kwa kifungu hicho kumethibitisha maneno niliyoyatoa bungeni kuwa tumefika hapa
tulipo kutokana na ‘uzembe wa bunge na wabunge’ na kwa hili pamoja na mchango
nilioutoa bungeni kwa maandishi siku hiyo juu ya haja ya kuwa mfumo mpana zaidi
wa pensheni na hifadhi ya jamii (universal pension and social security) pamoja
na kuwa sikuunga mkono kifungu husika kilichoingizwa kinyemela naomba radhi kwa
wananchi wa Ubungo na wafanyakazi kwa kutokuwasilisha jedwali la marekebisho
kupinga kifungu hicho kuingizwa.
Izingatiwe
kuwa ili kurekebisha hali hiyo tarehe 27 Julai 2012 kwa nafasi yangu ya Waziri
Kivuli wa Nishati na Madini kwa niaba ya Kambi Rasmi ya Upinzani niliitaka
Serikali itoe maelezo maelezo kuhusu taarifa zilizotolewa bungeni tarehe 13
Aprili 2012 kuwa wafanyakazi ikiwemo wa migodini kupitia vyama vyao
walihusishwa kutoa maoni yaliyopelekea kufutwa kwa fao la kujitoa (withdrawal
benefits); suala ambalo Chama Cha Wafanyakazi wa Migodini (TAMICO)
kililikanusha.
Hata
hivyo, Waziri wa Nishati na Madini wakati wa majumuisho ya Hotuba yake tarehe
28 Julai 2012 hakutoa majibu yoyote bungeni kuhusu suala hilo hali ambayo
imesababisha migongano kuendelea katika migodi mbalimbali kuhusu madai hayo
hali ambayo kwa taarifa nilizozipata tarehe 1 na 2 Agosti 2012 inaweza
kusababisha migomo migodini. Kufutwa kwa fao la kujitoa kumelalamikiwa pia na
wafanyakazi na wadau wa hifadhi ya jamii katika Jimbo la Ubungo na katika taifa
kwa ujumla.
Hata
hivyo, suala hili na tukio husika litumike kama rejea ya bunge na wabunge
kuikatalia Serikali kuwasilisha marekebisho yenye athari kubwa kipindi cha
mwisho na hivyo wabunge kukosa fursa ya kupata maoni ya wananchi na pia Serikali
itakiwe kuomba radhi kufuatia kulipotosha bunge kuwa wadau wa hifadhi ya jamii
hususan wafanyakazi na vyama vyao walishirikishwa na kuridhia wakati ambapo
wamejitokeza na kukanusha madai hayo yaliyotolewa na Wizara bungeni.
Kwa
upande mwingine kufutwa kwa mafao ya kujitoa msingi wake haupo kwenye
marekebisho ya sheria yaliyofanyika tarehe 13 Aprili 2012 pekee bali ni udhaifu
katika mfumo mzima wa kisera na kisheria wa hifadhi ya jamii nchini hali ambayo
inahitaji wadau kutaka mabadiliko makubwa.
Hivyo,
naungana na wote wenye kutaka Mamlaka ya Usimamizi na Udhibiti wa Sekta ya
Hifadhi ya Jamii (SSRA) kutengua taarifa kwa umma iliyotolewa ya kueleza kuwa
“kufuatia kuanza kutumika kwa Sheria hiyo (ya 13 Aprili 2012) maombi mapya ya
kujitoa yamesitishwa kwa kipindi cha miezi sita hadi pale miongozo
itakapotolewa ili kuwezesha Mamlaka na Mifuko ya Hifadhi ya Jamii kutoa elimu
kwa Wadau”.
Aidha,
pamoja na Mamlaka kueleza kwamba sitisho la fao la kujitoa si kwa sababu za
Kiserikali au Mifuko kufilisika ni vizuri mamlaka ikaeleza kwa uwazi na ukweli
sababu zingine za kufanyika kwa marekebisho hayo zaidi ya ile ya kutimiza
malengo ya Hifadhi ya Jamii ambayo ni kuhakikisha kuwa Mwanachama anapostaafu
anapata mafao bora yatakayomwezesha kumudu hali ya maisha ya uzeeni. Tahadhari
za Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) katika taarifa za Hesabu za mwaka
2010/2011 na miaka mingine zinaashiria masuala ya ziada ambayo yanaweza kuwa
yameisukuma Serikali kuja na mbinu zingine za kuhakikisha uendelevu wa mifuko
ikiwemo kupitia marekebisho ya sheria za hifadhi ya jamii.
Ili bunge
liweze kutimiza wajibu wa kuishauri na kuisimamia serikali kufanya marekebisho
yanayostahili ya sheria husika kwa haraka ni muhimu ratiba ya bunge
ikabadilishwa.
Tafsiri
ya marekebisho ya ratiba yaliyofanyika ni kuwa hoja binafsi niliyoiwasilisha
kwa katibu wa Bunge kutaka bunge lijadili na kupitisha maazimio ya hatua za
haraka za kuboresha upatikanaji wa majisafi na ushughulikiaji wa majitaka
haitapata nafasi ya kujadiliwa bungeni. Aidha ratiba hiyo mpya hoja binafsi
iliyoelezwa kuwa itawasilishwa na Mbunge wa Kisarawe Seleman Jafo kuhusu
kufutwa kwa mafao ya kujitoa kufuatia marekebisho ya sheria za Hifadhi za Jamii
nayo haitawasilishwa kwenye mkutano huu wa Bunge unaoendelea kama ratiba haitafanyiwa
marekebisho.
Hata
hivyo, izingatiwe kuwa chanzo cha kufutwa kwa mafao ya kujitoa ni marekebisho
ya sheria za hifadhi ya jamii hivyo ufumbuzi wa kurejesha fao la kujitoa
unapaswa kuwa ni marekebisho ya sheria hatua ambayo njia ya haraka ya kuifikia
ni kuwasilishwa kwa muswada wa sheria ama na serikali au kamati au mbunge
badala ya hoja binafsi.
Hoja
binafsi inaweza kuwezesha bunge kujadili na kupitisha maazimio ya kuitaka
Serikali kuwasilisha marekebisho ya sheria au kuishauri na kuisimamia serikali
na mamlaka zake katika utekelezaji wa sheria lakini sheria itaendelea kuwa
palepale mpaka marekebisho yatakapofanywa kwa kuwasilishwa muswada wa sheria
hatua ambayo nimeamua kuanzisha mchakato wa kuwezesha ichukuliwe.
Wenu
katika kuwawakilisha wananchi,
John
Mnyika (Mb)
Wednesday, August 1, 2012
MTOTO WA GHADAFI ATAKA SHITAKIWE ICC.
![]() |
| Saif al- Islam |
Mtoto wa marehemu Ghadafi Saif al-Islam alisema iwapo kesi yake itaendeshwa Libya basi inakuwa
sawa na kuuawa, kwa mujibu wa nyaraka zilizowasilishwa mahakama ya ICC(International Criminal Court).Kijana
huyo mwenye umri wa miaka 40 anashikiliwa na wapiganaji mjini Zintan. Amekuwa
akishikiliwa Libya tangu Novemba 2011Alishtakiwa na ICC kwa uhalifu dhidi ya
ubinadamu.
Serikali
ya mpito ya Libya mpaka sasa imekataa kumkabidhi Saif Uholanzi ambako mahakama
ya ICC iko ikisema kuwa hana budi kukabiliana na mashataka yake nchini Libya.Kanali
Gaddafi, ambaye utawala wake wa kidikteta ulidumu kwa miaka 42 aliuawa katika
mazingira ya kutatanisha baada ya kukamatwa na waasi mwezi Octoba, katika
kitendo ambacho kilishutumiwa vikali na makundi ya haki za binadamu.
'Ulinzi wa bandia'
"Siogopi
kufa lakini ikiwa itaendeshwa hapa hiyo muuite tu kuwa ni uuaji na
mmalizane," Saif al-Islam alinukuliwa na mawakili akisema.Mwezi Juni,
wafanyakazi waliotumwa na ICC walikamatwa baada ya kukutana na Saif al-Islam,
na kushikiliwa kwa zaidi ya wiki tatu.Nyaraka zilizowasilishwa mahakamani
zinasema wakati wa mkutano huo afisa aliyejifanya mlinzi alimzuia mwanasheria
wa ICC kuchukua kiapo kutoka kwa Saif al-Islam.
"Mlinzi
huyo ambaye kimsingi ni Bw Ahmed Amer – mwanasheria anayezungumza lugha kadhaa
alijumuishwa kwenye timu hiyo makusudi kuwalaghai " nyaraka ziliandika,
kwa mujibu wa Reuters."Alirejea chumbani na (mkalimani wa ICC akiwepo)
alianza kupiga kelele kuwa maelezo hayo yalikuwa hatari sana, yamekiuka usalama
wa Libya na kwa Ulinzi wasingeyarudisha"Mkutano ulistishwa baada ya dakika
45 na nyaraka zao kuharibiwa, wakili alisema. Baadaye walikamatwa.
Hatua
hiyo ilionekana kuwa "kimyume cha sharia, uhaini na ukiukwaji wa taratibu
za usalama wa Taifa kwa ama Bw Gaddafi au washauri wake na kuonyesha kuwa
Gaddafi hataki kesi yake iendeshwe na mahakama za Libya." Walisema
mawakili kwenye nyaraka.
Maafisa
wa Libya walimshutumu wakili Melinda Taylor, aliyekuwa akiongoza ujumbe wa ICC,
kwa kuwa na vifaa vya upelelezi vikiwa vimeshikizwa kwenye barua ya Saif
al-Islam wakati wa mkutano.
TAARIFA YA ZITTO JUU YA TUHUMA ZA RUSHWA
![]() |
| Mh.Zitto Kabwe akiongea na Waandishi hapo jana |
Ndugu
Waandishi,
Nalazimika
kukutana nanyi kutoa maelezo juu ya tuhuma zenye shinikizo la kisiasa
zinazoelekezwa kwangu binafsi kwamba hata mimi nimeshiriki katika vitendo vya
rushwa, kwa nafasi yangu kama Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Mashirika ya
Umma. Taarifa hizo, kama kawaida ya uzushi mwingine wowote zimesambazwa kimkakati na kwa kasi kubwa
kiasi cha kuukanganya umma.
Nafahamu
nabeba dhamana kubwa ya uongozi, taswira yangu ya uongozi daima imeakisi njozi
na matumaini ya wananchi wa Kigoma Kaskazini, wananchi wanyonge na vijana kote
nchini bila kujali itikadi zao za kisiasa, jinsia zao, makabila yao na rika
zao. Hivyo, nawajibika kupitia kwenu kuwatoa hofu juu ya hisia potofu
zinazopandikizwa kwao na wale wasiopenda kuona baadhi yetu tukiwaunganisha na
kuwasemea watanzania wasio na sauti, dhidi ya vitendo vya hujuma na vyenye
dhamira ovu kwa taifa.
Mkakati
huo wa kuniunganisha na baadhi ya Waheshimiwa Wabunge wanaotuhumiwa kwa kupokea
Rushwa unatekelezwa kwa njia zifuatazo:
1.Kumekuwa na kauli za watendaji wa
serikali ambao wamekuwa wakizieneza na hususan kutoa taswira kwamba baadhi ya
kauli zangu zinatokana na ushawishi wa rushwa;
2.Kuna taarifa ambazo zimeandikwa tena
katika kurasa za mbele za baadhi ya vyombo vya habari zikidai ’’Zitto kitanzini’’ ama ’’Zitto sawa
na popo nundu’’ zikiashiria kwamba na
mimi ni mla rushwa; na
3.Waandishi wa habari na jamii kwa ujumla
wamefikia kuaminishwa habari hizi kiasi cha wengine kuuliza kwa nini Mhe. Zitto
Kabwe hakutajwa katika orodha iliyotolewa na Mnadhimu Mkuu wa Kambi ya
Upinzani.
Ndugu
Waandishi,
Naomba
kutoa ufafanuzi wa hicho kinachoelezwa kwamba nina ushiriki katika masuala ya
rushwa hususan kwenye masuala yanayohusu sekta ya Nishati na Madini:-
1. Mara baada ya bodi ya Wakurugenzi ya Shirika la Usambazaji wa Umeme Tanzania
(TANESCO) chini ya Uenyekiti wake Meja Jenerali Mstaafu Robert Mboma kutangaza
kwamba imemsimamisha kazi Mkurugenzi Mkuu wa Shirika hilo, Nd. William Mhando
ili kupisha uchunguzi wa baadhi ya vitendo/mwenendo wake, Kamati ya Hesabu za
Mashirika ya Umma (POAC) ambayo mimi ni Mwenyekiti wake ilimuandikia Mhe. Spika
kumuomba aridhie ili Kamati iweze kuwaita Bodi ya TANESCO, Mdhibiti na Mkaguzi
Mkuu wa Mahesabu ya Serikali (CAG) na
pia Mamlaka ya Udhibiti wa Manunuzi ya Umma (PPRA) kujiridhisha na tuhuma zote
zinazotajwa zinafanyiwa uchunguzi wa kina na hatua kuchukuliwa;
2. Kamati ya POAC ninayoiongoza ilimuomba Mhe.
Spika kuwaita wahusika tajwa kwa kuwa zilikuwapo tetesi kuwa kusimamishwa kazi kwa
Mkurugenzi huyo siku chache kabla ya Bajeti ya Wizara ya Nishati na Madini
kulikuwa na lengo la kufunika ’madudu’ makubwa zaidi kwa kulichagiza Bunge na
tukio hilo dogo, mkakati ambao naona umefanikiwa sana. Isitoshe, Kamati kutaka
kujiridhisha na hatua za Bodi ni sehemu ya msingi ya utekelezaji wa majukumu ya
Kamati yaliyowekwa kwa mujibu wa Kanuni za Kudumu za Bunge na pia Shirika la
TANESCO ni moja kati ya mashirika ambayo yanawajibika kwetu kwa hesabu zake na
pia ufanisi wake kwa ujumla. Tumefanya hivyo pia katika mashirika mengine, hili
la TANESCO sio tukio la kipekee;
3.Kitendo hiki cha halali na kwa mujibu wa
Kanuni kilichofanywa na Kamati yangu
kimetafsiriwa kwa makusudi na baadhi ya watu kwamba ni ishara ya kuwa
sisi au zaidi kwamba mimi nina maslahi binafsi na TANESCO na hususan Mkurugenzi
wake Injinia Mhando, ndio maana tumetaka maelezo ya Bodi. Ukweli kwamba Kamati
ya POAC tumewaita pia Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Mahesabu (CAG) na Mamlaka ya
Udhibiti wa Manunuzi ya Umma (PPRA) kwa jambo hilo hilo umefichwa kwa makusudi!
4.Baada ya
tukio hilo, nikiwa hapa Dodoma, mwandishi wa habari wa gazeti moja
alinifuata akiniambia kuwa wamekutana na Mhe. Waziri Mhongo na Katibu Mkuu
wake, Nd. Eliachim Maswi hapa hapa Bungeni na wamewaambia kuwa mimi nimepewa
rushwa. Hakutaja nimepewa rushwa na nani, kiasi gani na wala kwa lengo gani!
5.Nimejaribu kumtafuta kwa simu Mhe. Waziri
Mhongo na Katibu Mkuu wake ili wanipe ufafanuzi juu ya mimi na Kamati ya POAC
kuhusishwa na tuhuma hizi bila mafanikio, hali ambayo inaniondolea mashaka juu
ya ushiriki wao katika kueneza au kuthibitisha uvumi huo. Najaribu sana
kujizuia kutokuwa na mashaka na ushiriki wao huo ikizingatiwa uzito na taswira
ya nafasi zao katika jamii, lakini wameshindwa kunidhihirishia tofauti.
Sasa
naomba kutoa ufafanuzi rasmi kuhusu mlolongo wa matukio hayo tajwa ambayo
yanatumiwa na baadhi ya wanasiasa kuonesha kwamba eti nimehusika na vitendo vya
rushwa.
1.Binafsi sijawahi kuwa na mawasiliano ya
aina yeyote na uongozi wa TANESCO kushawishiwa juu ya hatua ambazo POAC ndio
imezichukua za kutaka kujiridhisha juu ya utaratibu uliotumika. Ieleweke wazi
kabisa kuwa, hakuna wakati wowote, popote ambapo mimi binafsi au Kamati yetu
imekataa Mkurugenzi Mkuu wa TANESCO kuchunguzwa kwa tuhuma zozote. Ambacho
tumesisitiza wakati wote ni ufuatwaji wa taratibu, kanuni na sheria, hili
nitalisimamia iwe masika au kiangazi;
2.Ni kwa sababu hiyo, na kwa kujiamini kabisa
nimeunga mkono suala la tuhuma za rushwa zinazotajwa zichunguzwe na Kamati ya
Haki, Maadili na Madaraka ya
Bunge kwa kina;
3.Nimekwenda mbali zaidi kukiomba chama
changu CHADEMA kifanye pia uchunguzi na tathmini yake kwa kina kujiridhisha na
tuhuma hizo;
4.Natumia fursa hii pia kuomba vyombo vya
Dola vichunguze tuhuma hizo kwa nafasi yake ili kuweza kupata ukweli;
5.Ninaahidi kushiriki kikamilifu iwapo
nitatakiwa katika uchunguzi wowote utakaofanywa na niko tayari kuwajibika iwapo
nitakutwa na hatia yeyote.
Napenda
niwatoe hofu wananchi wa jimbo la Kigoma Kaskazini walionituma kuja
kuwawakilisha hapa Bungeni na Watanzania wote kwa ujumla kwamba:-
Mimi Zitto Zuberi Kabwe sina bei, sijawahi
kuwa nayo na sitarajii kuwa nayo huko mbeleni. Daima nimesimamia kidete maadili
ya uongozi bora katika maisha yangu yote ya siasa, na nawaahidi sitarudi nyuma
katika mapambano dhidi ya rushwa katika nchi hii pamoja na mikakati ya aina hii
ya kunidhoofisha na kunivunja moyo;
Nafarijika na salam mbali mbali
zinazotolewa kunifariji na kusisitiza kuwa nisilegeze kamba katika mapambano
haya, nimepokea ujumbe mwingi kwa simu, sms, tweeter na hata facebook na niko
pamoja nanyi Watanzania wenzangu kamwe sitarudi nyuma hadi kieleweke. Naamini
katika nchi yetu tunazo rasilimali za kutosha mahitaji/haja ya kila mmoja wetu
lakini si ‘tamaa/ulafi’ wa baadhi ya watanzania wenzetu;
Napenda kuweka rekodi sawa kwa Watanzania
kwamba nimekuwa Mbunge hiki ni kipindi cha pili, Mimi ni Mwenyekiti wa Kamati
ya Hesabu za Mashirika ya Umma (POAC) huu ni takriban mwaka wa saba sasa,
Kamati yangu inasimamia mashirika 259 ya Umma na si TANESCO peke yake. Mchango
wa Kamati hii katika Bunge na kwa ustawi wa Mashirika ya Umma ni bayana na
haujawahi kutiliwa shaka. Kamati yetu imeokoa upotevu mkubwa wa mali za umma na
kuokoa fedha za umma kutokana na umakini wake. Tumefanya hivyo CHC hivi
karibuni, Kiwira na kwenye mashirika mengine mengi. Kote huko uadilifu na
uzalendo wa Kamati hii haujawahi kuhojiwa. Inatuwia vigumu kuona kuwa
tunahojiwa katika suala hili la TANESCO. Hapa pana kitendawili.
Zipo hoja pandikizi za kutaka Kamati ya
POAC ivunjwe na haswa zikinilenga mimi binafsi. Nafahamu kiu ya wasioitakia
mema nchi yetu kuiona POAC ikivunjwa au sura zikibadilishwa kwa kuwa Kamati hii
imekuwa mwiba kwa mikakati yao ya kifisadi. Kwa maoni yangu, Kamati ya POAC
isihusishwe na tuhuma hizi kwa vyovyote vile. Niko tayari nihukumiwe mimi kama
mimi na sio kuhusisha wajumbe wengine ambao hawatajwi mahala popote katika
tuhuma hizi mbaya sana katika historia ya Bunge letu. Nitakuwa tayari kunusuru
Kamati ya POAC na maslahi ya taifa letu kwa kujiuzulu Uenyekiti iwapo
itathibitika pasipo shaka kuwa nimehongwa. Kamati ya POAC ni muhimu zaidi
kuliko mimi.
Nafahamu pia kuwa kuna wanasiasa hasa wa
Upinzani ambao wanautaka sana Uenyekiti wa POAC na wanafanya kila njia kutaka
kuidhoofisha. Lakini hawajui kuwa anaepanga wajumbe wa Kamati ni Spika wa
Bunge.
Msishangae pia kuja baadae kubaini kwamba
baadhi ya wanasiasa wenye midomo mikubwa ya kutuhumu wenzao wao ndio vinara wa
kupokea rushwa.
Ni lazima tufike mahali kama viongozi
kwamba utaratibu unapokiukwa na yeyote yule, au uongo unapotolewa hadharani
tuseme bila kuogopa. Hili ndio jukumu letu kama wabunge na viongozi. Kusimamia
ufuatiliaji wa utaratibu ni jukumu letu kama Kamati ya POAC na ndio sababu ya
msingi ya kuanzishwa kwa mamlaka kama CAG na PPRA. Haiwezekani, tuwe na set ya
kanuni kwa kundi fulani na nyingine kwa makundi mengine, au kuhukumu ufuataji
wa taratibu kwa kuangalia sura ya mtu usoni
Mwisho
Kumejengeka
tabia hivi sasa ya kuwamaliza wanasiasa wenye kudai uwajibikaji na uzalendo.
Kumeanzishwa kiwanda kwenye medani ya siasa cha kuzalisha majungu na fitna
zenye lengo la kuwachonganisha wanasiasa wa aina hiyo na wananchi kwa kutumia
vyombo vya habari na nguvu ya fedha. Naamini mbinu hizi chafu, kama nyingine
nyingi zilizojaribiwa kwangu huko nyuma nazo zitashindwa.
Naamini
katika kweli na kweli daima huniweka huru. Naamini kuwa mwale mdogo wa mwanga
wa mshumaa hufukuza kiza. Kwa imani hiyo, sitasalimu amri mbele ya dhamira zao
ovu hata nitakapobaki peke yangu katika mapambano hayo ya kulinda na kutetea
rasilimali za taifa zinufaishe watanzania wote.
Daima
nitaongozwa na busara ya Hayati Shabaan Robert isemayo, ‘Msema kweli huchukiwa
na marafiki zake, nitakapofikwa na ajali hiyo, sitaona wivu juu ya wale wawezao
kudumu na marafiki zao siku zote, siwezi kuikana kweli kwa kuchelea upweke wa
kitambo, nikajitenga na furaha ya kweli itakayotokea pale uwongo
utakapojitenga”.
Ahsanteni
sana.
Subscribe to:
Posts (Atom)




